SERIKALI imeanza kukipigia ‘debe’ Kiwanda cha Maziwa cha Tanga Fresh, kupata lita 80,000 za maziwa kila siku kutoka kwenye vikundi vya wasindikaji wa maziwa waliopo katika mkoa wa Kilimanjaro.
Hatua hiyo inafuatia kiwanda hicho kudai uwezo wake umeimarika maradufu tangu Rais John Magufuli alipoamuru kupatiwa kibali kilichokwama kwa muda mrefu.
Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdalah Ulega alisema jana hakuna sababu ya wazalishaji wa maziwa kulalamika kukosa soko, kwa kuwa hivi sasa kiwanda hicho kinasindika maziwa lita 120,000 na kinakabiliwa na upungufu wa lita 80,000 kwa siku.
“Naagiza ma DC (wakuu wa wilaya) na maofisa mifugo, simamieni na kuhamasisha wananchi kuunda vikundi vya wasindikaji wa maziwa, Tanga Fresh inasubiri maziwa kutoka kwao, kuna soko kubwa la maziwa na hakuna sababu ya wafugaji na wakulima wadogo kulalamika wanamwaga maziwa kwa kukosa soko,”alisema.
Hata hivyo, licha ya Tanzania kuwa nchi ya tatu Barani Afrika kwa kuwa na idadi kubwa ya mifugo, bado sekta ya maziwa haijaweza kutoa mchango mkubwa katika kuchangia pato la taifa huku mwamko wa wananchi katika unywaji wa maziwa ukiwa duni.
Kutokana na hali hiyo, serikali imeandaa kampeni ya okoa jahazi, jenga afya, jenga uchumi kupitia maziwa inayolenga kuleta mapinduzi katika sekta ya maziwa.
Miongoni mwa wafugaji wa ng’ombe wa maziwa watakaonufaika na soko hilo ni wale wanaouza mazao yao katika Kiwanda cha Kusindika Maziwa cha Kondiki kilichopo Marangu.
Jisajili kwenye:
Chapisha Maoni (Atom)
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni